Na. Lina Sanga
Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Mji Makambako,limetoa ushauri na maoni kwa Serikali juu ya namna ya kuwadhibiti simba hao,ikiwa ni pamoja na kuwatumia wawindaji kutoka jamii ya wamang’ati , wasaidie kuwawinda simba hao na kufanya maboresha ya mbinu za utafutaji wa wanyama wanaotoroka maeneo ya hifadhi ili kuwadhibiti mapema kabla hawajasababisha madhara makubwa.
Ushauri na maoni hayo yametolewa leo katika majadiliano baada ya kuwasilishwa kwa ajenda ya dharura ya uwepo wa simba wawili katika Halmashauri ya Mji Makambako, iliyowasilishwa katika Mkutano wa baraza la madiwani wa kuishia kipindi cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2022/2023,uliofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri.
Kwa nyakati tofauti Madiwani wamepongeza na kuishauri Serikali kupitia Wizara ya Maliasili kwa jitihada za kuwatafuta simba hao na kuitaka kuongeza nguvu zaidi ya kuwapata simba hao kabla hawajaleta madhara makubwa zaidi ,kwani wananchi wana hofu na shughuli za uzalishaji zimesimama kutokana na uwepo wa simba hao.
Awali akitoa taarifa hiyo Afisa Mazingira na Maliasili wa Halmashauri ya Mji Makambako, Gift Kiwia amesema kuwa,mnamo julai 29,2023 iliripotiwa uwepo wa simba wawili katika Mtaa wa Malombwe,Kata ya Lyamkena waliovamia na kuua ng’ombe 2,julai 30 walivamia na kuua nguruwe 1 na leo julai 31,2023 imeripotiwa uwepo wa simba hao katika Kijiji cha Mkolango,Kata ya Mlowa baada ya kuvamia na kuua ng’ombe 1 na nguruwe 2.
Ametoa rai kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhali kwani simba hao wanafanya uvamizi hasa nyakati za usiku,hivyo kwa wananchi wenye mifugo wajitaidi kuwasha moto usiku karibu na mazizi ya mifugo na kuwahakikishia kuwa skari 8 kutoka Mamlaka ya Uhifadhi wa Wanyamapori Tanzania(TAWA)wanafanya jitihada za kuwatafuta simba hao na kuwadhibiti.
Naye,Mkuu wa Wilaya ya Njombe,Mhe. Kissa Gwakisa Kasongwa amewataka wananchi wa Halmashauri ya Mji Makambako kuendelea kuchukua tahadhali ,kutokana na uwepo wa simba katika maeneo mbalimbali ndani ya Makambako,na kuwahakikishia kuwa Serikali ipo pamoja nao kwa kuhakikisha simba hao wanatafutwa na kudhibitiwa.
Makambako Town Council
Anuani ya Posta: P.O.BOX 405 Makambako
Simu ya mezani: 026-2730044
Simu ya Kiganjani: 0785635383
Barua pepe: td@makambakotc.go.tz
Haki miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Makambako. Haki zote zimehifadhiwa