Na. Lina Sanga
Njombe
Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka amezitaka Mamlaka za Halmashauri katika Mkoa wa Njombe kutumia takwimu za Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kubadilisha maisha ya wananchi.
Akizungumza na Madiwani, Wakurugenzi,Wakuu wa idara na Vitengo,Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji,Watendaji wa Kata,Mitaa na Vijiji wa Halmashauri za Wilaya ya Njombe katika Kikao kazi kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri ya Mji Njombe,Mhe. Mtaka amesema kuwa Mkoa wa Njombe unaongoza kuwa na idadi ndogo ya Watu Kitaifa tofauti na Mikoa mingine hivyo takwimu hizo zitakapochambuliwa kuanzia ngazi ya Kitongoji hadi Mji zitumike ipasavyo kupata idadi ya nguvu kazi ambayo itawezesha kubadilisha hali ya maisha ya Wananchi kwa kuwawezesha ili waweze kuzalisha na kukuza kipato chao na taifa kwa ujumla.
Amesema kuwa Mkoa wa Njombe wenye jumla ya watu 889,946 kupitia takwimu za Sensa ambazo zina taarifa sahihi za kila mwananchi mbali na watoto,watu wenye mahitaji maalumu na wazee kuna kundi la watu wenye nguvu ya kufanya shughuli za uzalishaji na kuongeza kipato chao.
Aidha ameongeza kuwa,ipo haja ya wananchi kubadilika na kuamua kufanya mapinduzi ya kiuchumi kwa kuachana na dhana ya kusaidiwa na Mfuko wa Maendeleo wa kaya masikini TASAF, kwani kwa miaka ijayo anatarajia watu wakatae kuandikishwa TASAF tofauti na hali iliyopo sasa ya baadhi ya watu kujenga chuki kwa Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji kwa kutoandikishwa kama wanufaika wa TASAF.
Pia ametoa wito kwa watumishi kutojihusisha na vitendo vya ulevi na visivyoendana na maadili ya kazi kwa kutambua umuhimu wa kazi na idadi ya wasomi wenye uhitaji wa ajira hizo.
Mkoa wa Njombe kwa Mujibu wa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka huu Mkoa wa Njombe una jumla ya wananchi 889,946 ambapo wanawake ni 469,413 na wanaume ni 420,533.
Makambako Town Council
Anuani ya Posta: P.O.BOX 405 Makambako
Simu ya mezani: 026-2730044
Simu ya Kiganjani: 0785635383
Barua pepe: td@makambakotc.go.tz
Haki miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Makambako. Haki zote zimehifadhiwa