Na.Lina Sanga
Tanga
Wakuu wa Mikoa wametakiwa kusimamia utaratibu wa ugawaji wa pikipiki kwa Maafisa elimu Kata wote Nchini,na kuhakikisha wanapata pikipiki hizo pasipo kujali uwezo wao wa kuendesha vyombo.
Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Ofisi ya Rais TAMISEMI,Mhe. Innocent Bashungwa leo wakati wa kufunga kikao kazi cha 17 cha Maafisa habari,Mawasiliano na Uhusiano wa Serikali mkoani Tanga.
Mhe. Bashungwa amesema kuwa wapo baadhi ya maafisa elimu wamezuia maafisa elimu kata, wasiokuwa na uwezo wa kuendesha pikipiki kukabidhiwa pikipiki zao kinyume na utaratibu,hivyo amewaagiza Wakuu wote wa Mikoa Nchini kusimamia zoezi la ugawaji wa pikipiki na Maafisa elimu Kata waruhusiwe kutafuta madereva wanao waamini wawaendeshe.
Wakati huo huo Mhe. Bashungwa amewataka Maafisa habari,Mawasiliano na Uhusiano Serikalini kutekeleza majukumu yao licha ya changamoto za ukosefu wa vifaa na bajeti zinazowakabili,Ofisi ya Rais Tamisemi kwa kushirikiana na Ofisi ya Utumishi kupitia Makatibu wakuu watatafuta fedha kwa ajili ya vifaa na kutambua umuhimu wa maafisa hao katika utendaji kazi wa Serikali.
Aidha amewataka Maafisa habari wa Serikali kutumia mbinu mbalimbali walizofundishwa kwenye kikao hicho,kwa kuleta mabadiliko kwenye utendaji wao wa kazi lakini pia kutokaa kimya katika utoaji wa taarifa kwa Umma kwa Wakati na kujibu hoja mbalimbali zinazotolewa na wananchi.
Mwisho amewataka Maafisa habari wote Nchini kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa zoezi la Sensa ya watu na makazi,kwa kuhakikisha kila mwananchi makazi yake yanasomeka kwenye mfumo wa anwani za makazi,lakini pia kila mwananchi ajiandae kushiriki zoezi la Sensa ya Watu na makazi Mwezi agosti 23,2022 ili Serikali iweze kupata takwimu sahihi ya watu na makazi.
#Jiandae kuhesabiwa
Makambako Town Council
Anuani ya Posta: P.O.BOX 405 Makambako
Simu ya mezani: 026-2730044
Simu ya Kiganjani: 0785635383
Barua pepe: td@makambakotc.go.tz
Haki miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Makambako. Haki zote zimehifadhiwa