Na. Lina Sanga
Wananchi wa Kijiji cha Ikelu.Kata ya Utengule katika Halmashauri ya Mji Makambako wameishukuru Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwa kutoa fedha zaidi ya Mil 264, zilizotumika katika ujenzi wa majengo matatu, jengo la wagonjwa wa nje,jengo la mama na mtoto na nyumba pacha za watumishi.
Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kijiji cha Ikelu,Mwenyekiti wa kijiji hicho Bw. Batson Nyagawa amesema kuwa,ujenzi wa Kituo hicho utawapunguzia wanachi mzigo wa gharama za matibabu kwani kwa sasa Kijiji cha Ikelu kina hospitali ya shirika la dini moja ambayo gharama za matibabu zipo juu tofauti na gharama katika hospitali na vituo vya Serikali.
Jengo la wagonjwa wa nje(OPD) na jengo la huduma ya mama na mtoto - Kituo cha Afya Ikelu.
“Kwa sasa wananchi wengi wasio na uwezo wanalazimika kusafiri kilomita 17 kufuata huduma za afya Kituo cha afya Makambako,kwa sababu hopsitali binafsi tuliyonayo gharama za matibabu zipo juu sana tofauti na zinazotolewa Makambako kwenye kituo cha Serikali,hivyo pindi ujenzi wa Kituo hiki utakapo kamilika wananchi watapata huduma zote hapahapa,”alisema Nyagawa.
Anna Mbangala,Mkazi wa Kijiji cha Ikelu na Mjumbe wa Serikali ya Kijiji amesema kuwa,ujenzi wa kituo cha afya katika Kijiji hicho una manufaa kwa jamii hasa kina mama kwani itawapunguzia gharama ya kupata huduma za uzazi,kwani kwa sasa mama mjamzito anatakiwa kulipia gharama za kujifunga kawaida kuanzia 50,000 na 250,000 upasuaji, hali inayowalazimu kufuata huduma hiyo Kituo cha afya Makambako kwani hakuna gharama zaidi ya kununua vifaa.
Nyumba pacha ya watumishi wa Afya Kituo cha Afya Kijiji cha Ikelu.
Mtendaji wa Kijiji cha Ikelu,Galous Myinga amesema kuwa hapo awali lengo lilikuwa kujenga Zahanati ya Kijiji kabla ya Serikali kuamuwa kujengwa kwa Kituo cha afya na walianza ujenzi wa majengo matatu ya rasmi mwezi april,2022 kupitia michango ya wananchi ambapo kwa wakati huo walifanikiwa kukusanya jumla ya Mil 16.7 na endapo wangejenga kupitia Michango ya wananchi pekee ujenzi hadi sasa ungekuwa hatua ya Msingi.
Ametoa shukurani kwa Serikali kwa kutoa fedha zilizofanikisha ujenzi wa majengo hayo,ambayo kwa sasa yapo hatua ya ukamilishaji pamoja na kuipandisha hadhi Zahanati hiyo Kuwa Kituo cha afya.
Mratibu wa TASAF katika Halmashauri ya Mji Makambako,Neema Chaula amebainisha Kutokana na mabadiliko ya Ujenzi wa Kituo cha afya badala ya Zahanati, Serikali Kupitia TASAF inatarajia kuongeza idadi ya majengo ya kutolea huduma ikiwa ni pamoja na jengo la upasuaji,Maabara na wodi ya mama na mtoto kwa gharama ya Mil. 135.
Makambako Town Council
Anuani ya Posta: P.O.BOX 405 Makambako
Simu ya mezani: 026-2730044
Simu ya Kiganjani: 0785635383
Barua pepe: td@makambakotc.go.tz
Haki miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Makambako. Haki zote zimehifadhiwa